Utashi wa Mungu na Upendo wa Mungu - Luisa Piccarreta
41 subscribers
285 photos
54 files
582 links
Fahamu kuhusu kutimia kwa Sala ya Baba Yetu kupitia Maandishi ya Mtumishi wa Mungu Luisa Piccarreta, Binti Mdogo wa Utashi wa Mungu - Kuishi Utashi wa Mungu
Download Telegram
Ewe Mtoto Wangu Mchanga na Laini, je unakiona, hicho kikosi cha kukupokea na kukusindikiza, nilichopenda kukuandalia, ili upate kukikuta wakati unapotoka tumboni mwa Mama? Kazi Zako zote zikiwa zimejipanga kama kikosi cha jeshi kinachokuzunguka Wewe, huyu msichana mdogo anapenda kukuambia Wewe na wanadamu wote: “Ninakupenda, Ninakupenda, Ninakupenda! Ninakuheshimu, Ninakushukuru, Ninakuabudu!” Na pamoja na watu wote ninapenda nibandike mhuri wa kauli yangu ya ‘Ninakupenda’ na nibandike pia busu langu la kwanza juu ya hiyo midomo yako inayotetemeka, wakati ukitoka tumboni mwa Mama na ukiwa unakimbilia kwenda kukumbatiwa na mikono ya Mama wa Mbinguni. Na yeye alikukumbatia sana na kukubana kifuani pake, alikubusu, na alipokupa maziwa yake unyonye alikupasha joto na kukutuliza usilie. Kwa jinsi nilivyo bado ni msichana mdogo mno, hata mimi napenda nikaingie pale katika mikono ya Mama nikumbatiwe, na juu ya busu lile lile analokupa, nami ninabandika busu la kwangu. Katika maziwa yake Mama, ninapenda kutiririsha ‘Ninakupenda’ yangu, kusudi, kama Mama anakulisha kwa maziwa yake, mimi nitakulisha kwa pendo langu. Kila kitendo anachokufanyia yeye Mama, nami napenda kukutendea hicho hicho. Ebu angalia, Ewe Mtoto Wangu Mpendwa, mimi hapa sipo peke yangu, nina kila kitu hapa: Lipo jua kwa ajili ya kukupasha joto, zipo hapa Kazi Zako zote kwa ajili ya kukutuliza usilie. Kwa minajili hiyo nipo nikifuatilia vilio vyako, malalamiko yako laini, na kwa vile unajiona hupendwi na wanadamu, mimi napenda niwe kama yaya Wako ili niwe ninakubembeleza kwa kukuimbilia: ‘Ninakupenda, Ninakupenda’ hata uweze kupata usingizi. Yote hayo ni kwa lengo kwamba mara nitakapokuona unashituka toka usingizini, mimi niwe ninakuomba Ufalme wa FIAT Yako.

Ewe Mama yangu, tafadhali unisaidie. Wewe, ukiwa pamoja na mimi, umwambie Mtoto huyu wa Kimungu: “Tafadhali umfurahishe huyu Binti yetu Mdogo ambaye hana kingine anachotaka na anachotamani na kulilia isipokuwa anaomba Utashi Wako ujulikane na utawale hapa duniani”.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba..
SAA YA KUMI

Tumfuate Mtoto Mchanga Yesu akiwa mikononi mwa Mama Yake wa Mbinguni, akiwa katika maumivu ya Kutahiriwa, na tufungilie tashi zote za kibinadamu ndani ya jeraha lake lenye maumivu
.
(Katika makala ya mkono hapa hufuata kile kilichoandikwa katika Juzuu Na. 17 - Hiki kinachofuata hapa chini ni kile ambacho kiliachwa kuandikwa katika Juzuu ile)

Ewe Mtoto Wangu Laini, kauli yangu ya ‘Ninakupenda’, ‘Ninakuheshimu’, na Ninakushukuru’ itakuwa inakufuata popote kwa ajili ya kukuomba FIAT Yako. Katika kila pigo la Moyo wako na katika kila pumzi yako, katika ulimi wako, katika mboni ya macho yako, kama vile matone ya damu yako yanavyojiongeza ndani ya Ubinadamu Wako mdogo, ndivyo na mimi nanuia kubandika mhuri wa ‘Ninakupenda’ yangu na busu langu juu ya kila moja ya mawazo yako matakatifu, juu ya mikono na juu ya viganja vya Mama wa Mbinguni na vya Mtakatifu Yosefu. Naweka huo muhuri kusudi hao wanapokubana kifuani pao, Wewe uwe unaionja ‘Ninakupenda’ yangu. Ninabandika muhuri hata katika pumzi za hao wanyama waliolala kimya hapo miguuni pako wakikupasha joto na kukuabudu kwa tendo lao la kufungua midomo yao na kucheua. Katika pumzi yao hiyo mimi napenda Wewe uwe unasikia ‘Ninakupenda’ yangu ambayo inakuomba FIAT Yako ya Kimungu.

Ewe Mtoto Wangu upendezaye na kuvutia sana, hiyo kauli yangu ya ‘Ninakupenda’ itakufuata hadi kule kwenye tendo la kukatwa kikatili wakati wa kutahiriwa. Katika ile Damu yako ya kwanza uliyomwaga, mimi nataka, kwa ‘Ninakupenda’ yangu, nipozeshe maumivu makali uliyopata. Juu ya kila tone la Damu hiyo, napenda kutia mhuri wa ‘Ninakupenda’ yangu, juu ya machozi yale uliyomwaga Wewe kutokana na maumivu, aliyomwaga Malkia Mwenye mamlaka kuu, na aliyomwaga Mtakatifu Yosefu walipokuwa wanakuona unavyoteseka. Damu ile, teso lile, na machozi yale, vyote vinaomba ushindi mkuu wa Ufalme Wako. Ewe Mpenzi Wangu Yesu Mdogodogo, napenda nikukumbatie kifuani penye moyo wangu ili nipozeshe maumivu na uchungu unaopata. Ndani ya hilo jeraha la kutahiriwa napenda kufungilia tashi zote za kibinadamu za wanadamu kusudi zisiwe na uhai wala ujimudu tena. Na kutoka katika jeraha hilo utokee sasa Utashi Wako wa Kimungu kuja kutawala kati yao wanadamu.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba..
SAA YA KUMI NA MOJA

Tunamfuata Mtoto Yesu anayekimbilia Misri. Tunaualika Uumbwa wote kuja kumbembeleza. Na pamoja nao wote tunaomba tuupate Ufalme wa Utashi wa Mungu.

Ewe Mtoto Wangu Mpendevu, pindi lile jeraha la kutahiriwa likiwa bado linatoa Damu, teso lingine zaidi laongezeka kukukabili Wewe: Ni mwuaji mkatili mmoja anayekutafuta ili kukuua. Wewe unapasika kwa lazima kutorokea Misri kwa ajili ya usalama wako. Hiyo ni tena ishara nyingine ya njama za utashi wa kibinadamu ambao unataka kuudhulumu Utashi Wako wa Kimungu ili kuuzuia usitawale.

Mtoto Wangu Maridadi, katika teso hili, ninapenda nitiririshe ‘Ninakupenda’ yangu, mabusu yangu ya upenzi, na pia utashi wangu ili usiwe na uhai tena, kwa ajili ya kuleta upatanisho na kujenga undugu baina ya utashi wa kibinadamu na Utashi wa Mungu na hatimaye kutengeneza Utashi moja tu. Na kwa nguvu ya hilo teso lako kali ninapenda nikuombe FIAT Yako. Basi kwa hiyo, pindi Mama anapokuwa amekubeba mikononi mwake, mimi ninafuata hatua za huyo Mama yangu. Na anapotembea, toka chini ya nyayo zake, ninapenda Wewe uwe unasikia ile kauli yangu ya ‘Ninakupenda’. Kwa sababu hiyo, hatua kwa hatua, juu ya kila atomu ya ardhi, juu ya kila unyasi au jani analokanyaga, mimi ninabandika hiyo kauli, na huku nikihamasisha mimi mwenyewe kwa sauti yangu, ninapenda Wewe uwe unasikia, toka pale kwenye nyayo za Mama yangu, kile kiitikio kinachosema: ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’. Na kama vile wewe unavyokimbia kwa lengo la kuniletea mimi uhai, mimi napenda nitoe uhai wangu uwe kwa ajili ya kutetea Uhai Wako, na napenda nikuombe sherehe ya ushindi wa Utashi Wako. Wakati huu unapokimbia, Ewe Pendo Langu, naonja moyo wangu ukipasuka, ninapokuona ukilia kwa uchungu, ukihema na ukitehemu. Moyo wangu unapasuka ninapoona jinsi unavyotafutwa, siyo kwa lengo la kukupatia mahali pa kulala, bali kwa lengo la kukuua. Mimi napenda nitulize machozi yako kwa pendo langu. Napenda pia kutwaa uwezo wa kuwa mahali mbalimbali katika Uumbwa kwa wakati ule ule. Kwa mfano, ili kukufurahisha, ninapenda usikie ‘Nakupenda’ yangu ikitokea toka kule ndani ya bahari. Mimi mwenyewe nikiwa ninahamasisha, kwa sauti yangu, matone yote ya maji, michezo yote ya samaki, napenda uwe unasikia ‘Ninakupenda’ ya viumbe vyote visivyo na sauti vinavyoishi pale baharini, na napenda usikie pia ule musiki wangu mzuri wa pendo, unaopita misiki yote, musiki wenye kile kiitikio changu: Ninataka FIAT Yako. Kwa wakati moja na uleule nataka niwe ndani ya Utashi Wako, juu ya ile milima mirefu kabisa, na katika mabonde yale ya kina kirefu. Nataka nikahamasishe mimea, maua, miti na mengine yote. Hao wote nataka wasikike wakisema: ‘Ninakupenda, Ninakupenda’. Juu ya mabawa ya Upepo ninapenda nikatengeneze sauti kali kupita zote ili Wewe uwe unasikia kauli ya ‘Ninakupenda’. Na katika mawimbi ya upepo nataka nipakie mabusu yangu motomoto na mapapaso yangu ya upenzi kwa ajili yako.
Ewe Mpenzi Wangu Mdogodogo, wakati wote unapotoroka, iwe usiku, iwe mchana, Wewe upo hadharani na unaonekana daima. Kwa hiyo ni vema tu kama mimi nipange kuviita vitu vyote vilivyoumbwa ili waje kumfurahisha Muumba wao. Basi ninaita sasa mwanga wote wa Jua. Unapoangazisha Uso Wako mzuri unatoa kauli kusema: ‘Ninakupenda’. Ninawaita na ndege wote waliopo angani, ili kwa nyimbo zao na sauti zao za kutetemesha, waweze kukutungia bembezi za pendo. Yaani tuseme, ninapenda nikupeleke hadi Misri ukiwa unasindikizwa na shangwe la ushindi la pendo langu, na kama kiitikio chake, ninakuomba Ufalme wa Utashi Wako. Sipo peke yangu, Ee Yesu, bali nipo pamoja na kazi zako zote. Je hivi husikii jinsi ilivyo nzuri na inavyopendeza: bahari, upepo, jua, nyota zinazometameta, vyote vikisema ‘Ninakupenda’? Anga, milima, mimea, vyote kwa pamoja na baina yao hupiga kelele kwa kadiri vinavyoweza vinasema: “Ninakupenda, Ninakupenda, tunautaka Utashi Wako unaotawala na unaoamrisha!”. Na mwangwi huo unasikika ukirudiwa katika kifua cha Mama Malkia na hata yeye anakuambia hivi: “Mwanangu, pendo langu hupatanisha na kuoanisha kila kitu, huunganisha tena vitu vyote, hushinda yote, na mwangwi huo unapopenya hadi ndani ya Moyo Wako, nao unakuomba FIAT Yako.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA MBILI

Tupo na Yesu pale Misri; tunamtolea moyo wetu uwe makao yake, na pamoja na Malkia wa Mbingu, tunaomba Ufalme wa Utashi wa Mungu.

Mpenzi Wangu Mtoto Yesu, wakati mimi bado ninakufuata nakuta umekwisha kuwasili tayari pale Misri. Natambua kuwa popote unakoelekea unafuatwa na mateso, na machozi, na kusahaulika, kuachika na watu wote, kiasi kwamba unapasika kuingia kujihifadhi katika kibanda kidogo na duni sana; hakijawahi kukarabatiwa wala kusafishwa, hakina madirisha. Kinapigwa na pepo na huwa kinavuja maji wakati mvua zinaponyesha. Hakuna hata mtu mmoja duniani hapa anayekupa malazi. Oh, ni jinsi gani unavyolalamika, Ewe Mtoto Wangu Mchanga kabisa, unapoona kuwa Ubinadamu Wako mdogo unakabili mkasa ule ule wa Utashi Wako Mwabudiwa, yaani, kwamba hakuna mtu ambaye, kwa ukarimu na uhuru wake, anatoa nyumba ya roho yake ili kuukaribisha Utashi wa Mungu na kuuruhusu utawale pale na kuamrisha. Ingawa kama umekwisha kufika kati yao, hata hivyo, unaonekana kuwa kama mtangatangaji tu. Kwa miaka zaidi ya elfu sita, amekuwa akiomba nyumba bila kufanikiwa kupata. Na Wewe, Pendo Langu, unalia kwa ajili ya mateso ya FIAT Yako ya Kimungu.

Ewe Mdogodogo Wangu wa Mbinguni, unaona kuwa Mama yetu, wakati anapolia pamoja Nawe, yeye anaficha machozi yake ili kunyamazisha kilio chako. Anatolea roho yake safi kabisa kabisa iwe ndiyo makao ya kudumu ya Utashi Wako wa Kimungu. Hata mimi ninafuatilia kilio chako. Ninapenda nipanguse na kukausha huo Uso Wako Mtukufu wa kupendeza. Nataka nibandike mhuri wa ‘Ninakupenda’ yangu juu ya kila chozi, juu ya midomo ile inayotetemeka na inayolalamika. Kadhalika napenda kubandika na busu langu la upenzi. Nataka kukuomba FIAT Yako na ninakutolea moyo wangu uwe kama makao ya kudumu daima ya FIAT Yako ya milele.

Mtoto Wangu Mpendwa, uliye makao makuu ya uhai wangu, wakati wote unapoishi katika kibanda hicho duni, ninapenda kufuatilia matendo Yako yote, nafuatilia pia matendo ya yule Malkia Mtawala Mkuu wa Mbinguni. Wakati yeye anakubembeleza kwa kukutikisatikisa, na mimi nitapenda kukubembeleza kwa kukutikisatikisa na kukuimbia ili upate usingizi. Wimbo wangu ni huu: ‘Ninakupenda, Ninakupenda’. Wakati anapokuandalia kashati kakukuvalisha, mimi, katika ule uzi anaopitisha katika vidole vyake vya kimama, wakati wa kushona, nataka nitiririshe humo ile kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuheshimu, Ninakushukuru, na Ninakuabudu’ kusudi wakati Mama yetu wa Kimungu atakapokuwa anakuvalisha, Wewe uwe unaonja kuwa vazi lako limeshonwa pamoja na ‘Ninakupenda’ yangu ambayo inakuomba FIAT Yako.
Ewe Moyo wa moyo wangu mdogo, wakati utakapoanza kujimudu na zile hatua za kwanza za kuyumbayumba, mimi napenda nitilie mhuri wa ‘Ninakupenda’ yangu, juu ya ile ardhi utakayokuwa unaikanyaga, ili kusudi uwe unasimama juu ya miguu yako mwenyewe. Na kwa mikono yangu, nitatengeneza uzio ili kukulinda na kukutegemeza usije ukayumbayumba na kuanguka. Ikitokea unayumba, mimi nitaweza kukukumbatia na kukubania kwenye moyo wangu. Ninagundua, Ewe Mtoto Wangu wa Mbinguni, kwamba mara baada ya kuacha kunyonya, na wakati huo ukiwa na uwezo wa kutembea mwenyewe, hata kama ungali bado ni kadogodogo, wewe unatoka na kujitenga na Mama kidogo, unapiga magoti yako madogo juu ya ardhi tupu, na huku ukipanua vimikono vyako vidogo, unasali, na unalia kwa ajili ya wokovu wa watu wote, na kwa kusihi sana na kuomboleza, unaomba Ufalme wa Utashi Wako wa Kimungu. Na kamoyo kako kadogo, kanapiga kwa nguvu kweli, kana kwamba kanataka kupasuka kwa sababu ya pendo na maumivu makali. Ewe Yesu Wangu Mdogo, ebu uniache tu mimi niweke kauli yangu ya ‘Ninakupenda’ hapo chini ya magoti yako madogo, kusudi hiyo ‘Ninakupenda’ yangu ilainishe na kulowesha kidogo hiyo ardhi isiwe kavu na ngumu mno kwa ajili ya viungo laini vya mwili wako. Tafadhali uniruhusu nitie mhuri wa ‘Ninakupenda’ yangu katikati ya mikono yako iliyopanuliwa na uniruhusu niishikilie hiyo mikono yako midogo miwili kwa mikono yangu ili usiteseke mno. Na wakati huo ninaposhikilia mikono yako, Wewe, Ee Mpenzi Wangu, unitwae mie kwa mikono yako hiyo midogo na unitolee kwa Baba wa Mbinguni, unitolee mimi Binti Mdogo wa Utashi Wako, huku ukinijalia nipate neema hii kwamba Utashi wa Mungu utawale ndani yangu mimi na ndani ya wanadamu wote.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA TATU

Tunashuhudia siku ile Mtoto Yesu Mpenzi, kwa mara yake ya kwanza, alipojitokeza nje kwa watoto wa Misri. Tunamshuhudia akiwabariki, na sisi tunamwomba Yeye, kwa njia ya Baraka Yake, atie mhuri juu ya tashi za kibinadamu.

Ewe Mtoto Wangu wa Mbinguni, Pendo Lako linakusukuma utoke nje ya kile kibanda kidogo na uende nje. Na watoto wa Misri, wakivutwa na uzuri wako unaopendeza, wanakusanyika kwa wingi kukuzunguka, na Wewe, kwa upendo mkubwa unazungumza nao. Wakiwa wametekwa Nawe, wao wanakusikiliza. Baada ya kuwafundisha unahitimisha kwa kuwabariki na halafu unatoka ukikimbia kwenda kwa Mama Yako kwani pendo lake linaleta mwangwi ndani ya moyo Wako.

Wakati naye Mama anapokuita Wewe unakimbilia mara mikononi mwake. Ewe Pendo Langu, mimi ninapenda kukufuata katika kila kitu kwani napenda iwe inasikika tena ile kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’. Kauli hiyo iwe inasikika chini ya hizo hatua zako nyepesi, isikike unapotembeza hiyo mikono yako midogo, isikike katika maneno yako matamu, pendevu, yenye nguvu ya kuteka akili, na yaliyojaa uhai.

Napenda isikike hata katika mtazamo wa macho yako yanayovuta na kupendeza. Na katika hayo yote ninakuomba Ufalme wa FIAT Yako. Wakati huo unapowabariki watoto, ubariki hata mimi Binti Mdogo wa Utashi Wako na kwa Baraka Yako, ugonge mhuri wa uhai wa Utashi Wako ndani ya hii roho yangu ndogo. Ninaendelea kukufuata, Ewe Mtoto wa Kimungu, wakati unapokwenda kufanya matembezi katika mashamba na pale unapofurahia kupita kuchuma maua. Unaponyosha mkono wako ili kuchuma maua, mimi ninakupenda Wewe na juu ya kila ua unalochuma, mimi napenda kurudia kile kiitikio changu cha ‘Ninakupenda, Ninakupenda’.
Hata hapo ninakuomba upeleke kwa Baba Yako wa Mbinguni hili ua dogo la huyu Binti Mdogo wa Utashi Wako, ili kusudi asiweze tena kujua, wala asiweze kupenda na wala kutaka kitu kingine chochote isipokuwa FIAT Yako ya milele.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA NNE

Tunamfuata Yesu ambaye, baada ya kukaa kama mkimbizi, sasa anarejea kwake Nazareti. Kwa kumnyeshea mvua ya kauli yetu ya ‘Ninakupenda’, tunamwomba, kwa sauti elfu na elfu, Ujio wa Ufalme Wake wa Kimungu.

Ewe Mtoto Yesu, Uhai Wangu, natambua kuwa kipindi chako cha kuwa mkimbizi kimemalizika na sasa unarejea Nazareti; na mimi nataka nikufuate hatua kwa hatua, yaani, napenda kuambatana nawe nikikusindikiza katika mvua inayokunyeshea kauli za ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, na Ninakuheshimu’. Kwa hiyo, ili niweze kusaidiwa, ninaita msaada wa mwanga wa Jua unyeshe ‘Ninakupenda’ kama mwanga. Ninaita na mmetuo wa nyota zote nao uinyeshe ‘Ninakupenda’. Na ule mvumo wa upepo, iwe ule wa sauti ya kulia, au upepo ule unaopiga kelele kali, au ule unaopiga kama miluzi, nao ninauita uinyeshe ‘Ninakupenda, Ninakupenda’. Ninawaita na ndege wote wanaoruka hewani, ili nao wakusindikize kwa musiki wao, kwa nyimbo zao, na kwa sauti zao za kutetemeshwa, zote zikisema: ‘Ninakupenda, Ninakupenda’. Ninawaita na hao kondoo wadogo, nao walie na kuita wakisema ‘Ninakupenda’. Naiita na bahari, nayo itoke na kuvuka toka kule kwenye ufukwe wake, ili ikusindikize kwa mawimbi yake ya ‘Ninakupenda’. Lakini, je wafahamu ni nini hasa, anachotaka huyu Binti Yako Mdogo anapokunyeshea mvua hii ya ‘Ninakupenda’? Nataka kitu kimoja tu: Ukubali kunipatia Ufalme wa Utashi Wako. Na wakati unapojifungilia pale kijijini Nazareti, mimi ninajifungilia pamoja Nawe, ili niwe ninaendeleza hii mvua ya ‘Ninakupenda’ yangu, ili kusudi nikushinde Wewe kwa njia ya pendo hata uweze kunipatia mimi kile ambacho Wewe Mwenyewe unataka, ambacho na Mama Malkia anataka na ambacho na mimi pia ninataka: Yaani, kwamba Utashi Wako upate kujulikana na upate kutawala kati ya wanadamu.

Ewe Yesu, Uhai Wangu, mimi sasa nipo tayari na Wewe, hapa katika nyumba hii ya Nazareti. Hatua kwa hatua napenda kukufuata ili niendelee kugonga mhuri wa ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’ juu ya kila kitu unachofanya Wewe, na ili kusudi nikuombe Wewe Ufalme wa Utashi Wako. Iwapo mikondo ya pendo inatiririka kati ya Wewe na Mama Yako, ndivyo pamoja nayo inatiririka ‘Ninakupenda’ yangu. Hiyo yote ni kwa kusudi la kuwaombeni Wewe na Mama wa Mbinguni kuwa Utashi Wako ujulikane. Kama Wewe unakula chakula, hapo na mimi nagonga ‘Ninakupenda’ yangu, ili kwa kauli hiyo nikuombe lishe ya Utashi Wako kwa ajili ya wanadamu wote. Unapokunywa maji, mimi natiririsha ‘Ninakupenda’ yangu ndani yake, ili kukuomba kwamba maji safi ya Utashi Wako, yatiririkie katika matumbo yetu, kwamba, ndani ya watu wote yakatengeneze mzunguko wa damu, ambayo, katika viungo vyote vya mwili wetu, itakuwa ikituwezesha kuonja uhai wa Utashi Wako wa Kimungu. Unapogonga mti au ubao wowote kwa mikono yako hiyo ya uumbaji, hapo unakuwa ukigonga ubao wa utashi wangu wa kibinadamu ili kusudi upate kuongokea katika mwanga wa Utashi wa Mungu.
Hiyo ‘Ninakupenda’ yangu inaendelea kukufuata Wewe. Wakati wa shughuli zako za ufundi seremala, unapotwaa misumari na nyundo katika mikono yako, ninakufuata, ili kwa njia ya ‘Ninakupenda’ yangu, niweze kukuambia hivi: Pigilia kwa misumari tashi zote za kibinadamu ili ziruhusu Utashi Wako uweze kuishi kwa uhuru. Wakati ule unaporudi na kuingia peke yako chumbani mwako kwa ajili ya kusali au kwa ajili ya kulala, mimi huwa sikubali kukuacha peke yako. Mimi huwa ninapenda kuwa pale kando yako, na endapo sipati kitu cha kukuambia, basi nitakuwa nikipwepa hapo sikioni pako nikisema: “Ninakupenda, Ninakupenda, Ninakupenda, Ninakuabudu”. Na kwa sala zako Wewe Mwenyewe, nitakuomba Ufalme wa FIAT Yako, na nitakuomba pia, kwa nguvu ya usingizi wako, uutie usingizini utashi wa kibinadamu, ili kusudi usiwe tena na uhai wowote, na badala yake, niwe ninaupata daima uhai wa Utashi Wako wa Kimungu peke yake. Ewe Yesu Wangu Mtukufu, mimi ningejionja uchungu sana iwapo kama nisingeweza kukufuata katika mambo yote, na kama nisingekuwa naendelea kukushughulisha na usindikizi wangu na kama nisingekufanya uwe unasikia daima kiitikio cha kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’, kwa ajili ya kukuomba Wewe, nikiwa pamoja na matendo Yako, Ufalme wa Utashi Wako. Ni kwa vile, ninapokuwa kando yako, mimi huwa ninaonja mapigo yale yale ya Moyo Wako, yaani ya kuwa nao huo Moyo Wako unataka kitu hicho hicho, na hata wenyewe Utashi Wako wa Kimungu, nao unataka ujulikane kwa watu, na unataka utawale na kuamrisha kati ya wanadamu.

Kwa sababu hiyo, ninakufuata hata unapokwenda Hekaluni. Wewe lakini, kwa tendo lako la kumwepa Mama Yako, ulikuwa umeleta maumivu makali na ya uchungu aliyoyakabili katika muda wa siku tatu za kupotea kwako. Mimi ninatiririsha ‘Ninakupenda’ yangu ndani ya lile teso la Mama yako na katika tendo la kupotea kwako, ili kusudi niombe kwamba utashi wa kibinadamu upotelee mbali. Kwa jinsi hiyo sisi, tunapokosa kuuona, tuwe tunaamua kuishi kwa Utashi wa Mungu na tuishi katika ile furaha ambayo ninyi, Mama na Mtoto, baada ya kupoteana, mliweza kuionja kwa karibu zaidi, pale mlipokutana tena. ‘Ninakupenda’ yangu inakuomba kwamba wanadamu wasikuletee tena uchungu na maumivu yale ambayo utashi wa kibinadamu huwa unakuletea mara kwa mara, lakini badala yake wawe wanakupatia furaha zilizo safi na raha mbalimbali zilizo nzuri kabisa za FIAT Yako ya Kimungu inayotawala ndani yao.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA TANO

Tumfuate Yesu kule jangwani. Tunapofika na kusimama pale kwenye mto Yordani, tumwombe atupatie Ubatizo wa wokovu wa Utashi wa Mungu ili kusudi watu wote waupate Uhai Wake.

Ewe Chema Changu Kikuu cha Mbinguni, mimi naharakisha kukufuata kwani vinginevyo muda hautanitosha kuweza kukufuatilia katika yote. Ninakuona tayari umejiandaa kutoka kwenda jangwani. Unamkumbatia Mama yako ukimbana kwenye Moyo wako unaoumia na kulia kwa pendo, na unamwambia: “Kwaheri, ubaki hapa, Ee Mama. Ninakuachia FIAT Yangu ya Kimungu, iwe hapa kama msaada kwako badala yangu, iwe kama uhai wako na kama mjumbe wa mawasiliano kati ya Mimi na Wewe’ . Utashi Wangu utakuwa unakuambia kila kitu atakachokuwa anatenda Mwanao, na wewe utakuwa ukinifuata katika kila kitu, kiasi kwamba, hata kama utakuwa mbali, FIAT itakuwa inakuleta karibu kabisa nami, hata tutajiona kuwa ni kitu kimoja tu”.

Ewe Yesu, nipe mkono wako na unichukue nije Nawe, ili chochote utakachokuwa unatenda kisiweze kunitoroka akilini mpaka niweze kufungilia ndani yake ile ‘Ninakupenda’ yangu, kwa ajili Yako, kusudi nikuombe Ufalme wa Utashi Wako wa Kimungu juu ya dunia. Kwa hiyo, wakati Wewe unaendelea kutembea peke yako, mimi ninakufuata hatua kwa hatua nikiwa nimebeba kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’. Katika kila pumzi yako nataka nikufanye uwe ukipumua ‘Ninakupenda’ yangu. Kila moja la neno lako nalifungilia ndani ya ‘Ninakupenda’ yangu. Katika kila mtazamo wa jicho lako nataka uwe unakutana na ‘Ninakupenda’ yangu. Na wakati unapowasili pale Yordani mimi napenda nitiririshe ‘Ninakupenda’ yangu ndani ya maji yale. Natiririsha kwa jinsi kwamba, kama vile Mtakatifu Yohane Mbatizaji alivyotiririsha maji kichwani pako kwa ajili ya kukubatiza, ndivyo sasa na Wewe uonje kuwa Binti Yako Mdogo kamwe hatakuacha peke yako bali anaambatana nawe kwa njia ya ‘Ninakupenda’ yake. Kwa kutiririsha kauli hiyo katika maji yale anataka akuombe Wewe utoe maji ya ubatizo ya Utashi Wako wa Kimungu kwa ajili ya wanadamu wote, ili huo uwe ndio mwanzo wa Ufalme Wake. Ewe Pendo Langu, katika tendo la kisherehe la Ubatizo wako, napenda nikuombe neema moja ambayo Wewe kwa uhakika hutanikatalia: Ninakuomba kwamba, kwa mikono yako mitakatifu, uibatize hii roho yangu ndogo katika maji yaletayo uzima na ya uumbaji ya Utashi Wako wa Kimungu. Ninaomba hilo ili kusudi roho yangu isionje kamwe, isione, na wala isiujue uhai mwingine isipokuwa uhai wa FIAT Yako. Ah, kweli kabisa, ninakuomba kwamba uwepo wangu usiwe ni kitu kingine, bali uwe ni tendo moja pekee la Utashi Wako.
Ewe Yesu Wangu, Pendo Langu tamu, mimi ninakufuata kwenda jangwani. ‘Ninakupenda’ yangu haitakuacha peke yako katika jangwa hili. Nitabaki kuwa kando yako usiku na mchana. Nitakapokuona, ukiwa na masikitiko sana, ukiwa na mahangaiko, unapokufa kwa pendo, na nitakapokuona ukisali na ukilia kutokana na upweke wa Utashi Wako wa Kimungu baada ya wanadamu kuutoroka, mimi nitabaki kando yako. Wewe unaonja mara moja na hai kabisa maumivu ya Utashi huu wa Kimungu, siyo tu kwa vile hautawali kati ya wanadamu, bali kwa vile Utashi huu umeachwa katika upweke mithili ya jangwani, ni kama umeachwa uhamishoni. Kwa hiyo Ubinadamu Wako Mtakatifu mno unalia na unaomba, kwa niaba ya familia yote ya binadamu, kwamba zile tashi mbili, yaani, ule wa Kimungu na ule wa kibinadamu, budi zikutane na zijipatanishe zenyewe. Utashi wa kibinadamu unauita Utashi wa Mungu, ili kuuruhusu uje utawale, na Utashi wa Mungu unasamehe juu ya kipindi kile kirefu, ambamo wanadamu walikuwa wameushika na kuuzuia uhamishoni. Mimi nayachukua machozi yako na kuyafanya yawe ni ya kwangu, sala zako ziwe ni za kwangu, vionjo vya kifo vya Moyo Wako unaoungua kwa pendo, navyo viwe ni vya kwangu. Naendelea kukifuatilia kila kitu kwa ‘Ninakupenda’ yangu. Natengeneza minyororo mitamu ya pendo, na ninaingiza nafsi Yako yote ya Kimungu ndani yake kwani ninataka nikuvute kwa lazima ukubali kunipa Ufalme wa Utashi Wako wa Kimungu hapa duniani. Ebu sikiliza Ewe, Uhai Wangu, mbona ni yenyewe mapigo ya Moyo Wako, ni matamanio yako Mwenyewe, ni machozi yako, ni maumivu yako, ndiyo hayo yanayotaka na yanayoomba Ufalme wa FIAT Yako. Kwa hiyo basi, endapo hutaki kunisikiliza mimi, basi nakuomba ujisikilize Wewe Mwenyewe, na unipe jibu kusudi tutoke katika jangwa hili huku ukiniambia hivi: “Ah, ndiyo basi! Ufalme wa Utashi Wangu utafika hapa duniani!”

Ewe Yesu Wangu, Moyo wa moyo wangu, ninakuona ukiharakisha mpango wa kutaka kutoka jangwani. Naona unapitia tena kule kwenye mto Yordani ili, kwa upendo, ukamchungulie tena mpenzi wako Yohane. Moyoni mwake unatia mafuriko ya pendo na neema, na halafu kwa haraka haraka unaendelea na safari hadi kuifikia nyumba yako ya Nazareti, ambako pendo la Mama wa Mbinguni linakuita kwa mfululizo. Na tazama, Oh, nini hiki ninachoshuhudia kikinivuta hapa mbele yangu! Mama na mtoto wanarukiana, huyu katika mikono ya mwenzake, na kwa kuyeyushiana, hawa wawili wanatengeneza pendo moja tu. Maadam Malkia wa Mbinguni amekuwa akionja hitaji kali mno la kumwona tena Mtoto wake. Moyo wake wa kimama ulikuwa umeunguzwa moto wakati huu alipokuwa hayupo, wakati yeye Mama alikuwa anatamani kujimwaga ndani ya Mwanae, ili aweze kupokea umande wa Pendo Lake, ili asibaki ameteketezwa na miali ile ya moto, iliyokuwa ikimtafuna. Na Yesu, Mkombozi Wangu wa Mbinguni, kwa upande Wake, alikuwa naye akionja hitaji kali sana ya pendo la Mama. Ni kwa sababu hiyo alirukia mikononi mwa Mama Yake kusudi akatoe pendo na kupokea pendo. Hata mimi, nikiwa nimeshika ule mwali mdogo wa moto wa ‘Ninakupenda’, narukia katika makumbatio yenu hayo yaliyo safi sana, narukia katika makaribiano yenu, narukia katika mioto ya pendo la Mama na Mtoto wake, na kwa wote wawili, Mama na Mtoto, ninawasihi ninyi nyote mnipatie Ufalme wa Utashi Wenu. Ewe Mama Mtakatifu, urudie pamoja nami na usali pamoja nami, kwamba Utashi wa Mungu ujulikane, utawale, hapa duniani kama kule Mbinguni.

Wakati huu ambapo Mama na Mtoto wanajipumzisha kidogo katika pendo lao na wakati wanapochukua uhai, papo hapo wanajiandaa kwa ajili ya kukabili hali ya kuachika ya kipindi kirefu zaidi. Tayari Yesu Wangu, ambaye daima mtu hawezi akamfikia katika kiwango cha Pendo Lake, anachukua njia ile inayoelekea kwenye maisha yake ya hadharani. Anamkumbatia kwa nguvu kabisa Mama Yake, kwenye moyo wake, kwa ajili ya kumtia nguvu huyu Mama, kwa mara nyingine anaaga na anatoka peke yake kabisa, kwa ajili ya kwenda kueneza Neno lake la Kimungu kwa mataifa, kwenda kuunda wafuasi wake, na kwenda kutangaza Injili Takatifu.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA SITA

Tumfuate Yesu kwenye Harusi ya Kana na pale tunamwomba augeuze utashi wa kibinadamu na aubadilishe na Utashi wa Mungu. Tuendelee kumfuata katika maisha yake ya hadharani.

Ewe Yesu, Pendo Langu na Uhai Wangu, ninatambua kwamba, kabla ya kuanza maisha yako ya hadharani, Pendo liwakalo la Moyo Wako linakuvuta kwenda kwanza kuhudhuria harusi ya Kana. Mimi, pamoja na Mama Yako, ninafuata hatua zako, nikiwa nimebeba ‘Ninakupenda’ yangu. Ninausikia Moyo Wako ukigonga kwa mapigo ya Pendo na maumivu.

Hapo unakumbuka harusi ile nyingine, iliyohudhuriwa na kubarikiwa Nawe pale katika Bustani ya Edeni. Ni ile ya Adamu na Eva walipokuwa hawana doa la dhambi. Ilikuwa ni ndoa katika nyanja mbili: kwanza ilikuwa ni ndoa kati ya Utashi Wako wa Kimungu na utashi wa kibinadamu, pili ilikuwa ni ndoa kati ya mtu mwanaume na mtu mwanamke. Katika ndoa hii, kama posa, Wewe uliutoa Uumbwa wote na hata Utashi Wako wa Kimungu ulio hai. Wewe uliutia Utashi Wako huo ndani ya moyo wao na ndani ya vitu vyote vilivyoumbwa.

Kwa minajili hiyo, uwepo Wako leo katika harusi hii, kitu kisichokuwa cha kawaida kwako, kunaniambia kwamba Wewe unapenda Utashi Wako wa Kimungu utawale, na unataka upange upya mambo yote ndani ya wanadamu.

Na mimi upande wangu, Ewe Yesu Wangu, nataka nije hapa kando Yako ili, katika mtazamo wako mtamu wa macho, katika sauti yako yenye musiki mtamu, na katika hiyo mitindo yako ya kuringa, niweze kujaza kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, na Ninakushukuru’. Kwa nguvu ya Pendo lile lililokusukuma Wewe uyapokee maombi ya Malkia wa juu mwenye mamlaka hata ukatenda muujiza wa kugeuza maji kuwa divai, mimi ninakuomba utende sasa, pia kwa pendo la Mama Yako wa Mbinguni, muujiza mkubwa wa kugeuza utashi wa kibinadamu uwe ni Utashi wa Kimungu, na uufanye huo Utashi wa Mungu utawale hapa duniani sawa kama kule Mbinguni.

Ewe Mama Mtakatifu, wewe uliyekuwa unahangaika sana kwamba Yesu ageuze maji kuwa divai, ili kuwasaidia wale wanaharusi, naomba usimwache Yesu atoke na kwenda kwenye utume wake wa hadharani, bila kwanza kukubali kwamba Utashi Wake ufike na utawale juu ya dunia.

Ewe Chema Changu Kitamu, hii kauli yangu ya ‘Ninakupenda’, pamoja na kale kawimbo bembezi endelevu, kwa ajili ya kukueleza kuwa ninataka Utashi Wako wa Kimungu utawale hapa duniani kama kule Mbinguni, hivyo havitakoma kamwe. Na ili kukulazimisha, nataka nikufuate katika kila kitu kusudi niweze kutia ‘Ninakupenda’ yangu katika matendo yako yote.

Nitaiweka hiyo ikuzunguke, ndani yako na nje yako, kama kikosi cha jeshi kali ili liwe linakupwepea sikioni mwako likisema: Ebu nipatie FIAT Yako hiyo inayogonga Moyoni Mwako, ebu nipe Utashi Wako huo unaozungumza ndani ya neno lako, Utashi huo unaotenda kazi mikononi mwako, huo unaotembea katika hatua zako, na ambao ndani ya nafsi yako nzima unakuambia: Ninataka Utashi Wako unaotawala hapa duniani kama kule Mbinguni. Lo, ebu umsikilize huyo Binti Yako Mdogo, ebu ujisikilize Wewe Mwenyewe, Wewe unayependa kwamba tuishi katika FIAT Yako!.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA SABA

Tumfuate Yesu katika maisha yake ya hadharani, katika miujiza yake, na tumwombe atende ule muujiza mkuu wa kuzifufua roho za watu katika Utashi wa Mungu.

Ewe Yesu Wangu, Uhai Wangu Mpenzi, ninakuona unapotoka na kuagana na Mama Yako. Lakini, tashi zenu hazitengani, bali, ni kwa vile tu unapasika kuaga ili ukaanze maisha yako ya hadharani. Miguu yako inaelekea Yerusalemu kwa ajili ya kwenda kufundisha Neno Lako takatifu pale Hekaluni. Na pale utawaambia wazi hadharani kwamba Wewe ndiye Yule aliye Masiha wa kweli wanayemtamani. Lakini, ni maumivu mangapi yanaingia Moyoni Mwako! Ni mateso mangapi! Wanaposikia mahubiri yako, badala ya wao kujitupa miguuni pako na kukupokea kama mwokozi wao wa Mbinguni, wao wanakuangalia kwa macho ya kutisha na ya chuki, wanakusikiliza huku wakinung’unika, kiasi kwamba hakuna hata mtu mmoja kati yao anadiriki kusogea na kukukaribisha akikuambia: “Njoo karibu nyumbani kwangu”. Wewe unaachwa mpweke! Kutokana na utovu wa shukrani kati ya watu wale, unapasika kuombaomba mkate, unapasika kuwa unatoka nje peke yako; tena ni lazima uwe unatoka usiku tu, kwani unalala sakafuni na wala huna cha kujifunika, bali unalala ukitazama nyota za angani wakati wote wa usiku. Nyota zile, kwa memetuko wao mzuri na wa taratibu, zinakusindikiza, na Wewe unapitisha usiku wote katika machozi na katika sala kwa ajili ya hao hao watu ambao hawataki kukujua.

Ewe Yesu Pendo Langu, ebu njoo hapa katika mikono yangu ili uweze kujipumzisha kidogo. Ninataka niwe ninalia na kusali pamoja Nawe, nataka nipange usindikizi wangu wa ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’ katika maumivu unayoyapata, katika machozi yako unayomwaga, katika maneno yako yasiyopokelewa. Nataka niweke ‘Ninakupenda’ yangu mbele ya hatua zako, nyuma na mbele ya hatua zako, ili kusudi miguu yako isiwe inaonja ugumu wa udongo usiokuwa na shukrani, bali badala yake iwe inaonja ulaini wa ‘Ninakupenda’ yangu na ninapenda nikuambie: Ewe Yesu, je waona jinsi unavyoteseka? Basi fanyiza ili Utashi Wako wa Kimungu utawale na ndipo maumivu yako yatakoma.

Yesu Wangu, Uhai wa moyo wangu duni, Pendo lako halisimami. Unaendelea kurejea Hekaluni na unaendelea kuwagawia watu Neno lako takatifu. Ingawa kama watu wakubwa na wasomi hawataki kukutambua na kukuheshimu, kundi kubwa la masikini, la wasiosoma, na wanaoteseka na maradhi mbalimbali, wanakukimbilia na kukusonga, wakiwa wanavutwa na mitindo yako ya upendo na wema, wakivutwa na sauti Yako yenye kuteka, kwani wanapokusikiliza ukizungumza huwa wanaonja kuguswa sana, na kuchomwa moyoni mwao. Ni hawa mafukara ndio wanafungua angalau mshipa wa furaha na raha ndani ya Moyo Wako. Kwa hoja hiyo, unaonja walau kwamba unaweza sasa kuwafariji, kuwafundisha, kuwaponya masikini ambao, wanahesabika kuwa kama takataka za jamii. Wewe unakuwa sasa ni rafiki, mwalimu, na mganga tabibu mwema wa masikini. Kwa hao wote Wewe unayo maneno ya faraja. Na kwa ajili ya kuwaponya, Wewe hunyanyapai kuvigusa viungo vyao vya mwili vilivyo na maradhi mbalimbali.

Unakwenda mji kwa mji, na mimi nataka nifuate hatua zako, ili nikaweke ile alama yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakushukuru, ninakuheshimu’ katika njia mbalimbali, na katika miji. Na mara kwa mara nitakuwa nakusogelea na kukubana mkononi nikikupwepea katika sikio Lako: Ebu unipe Ufalme wa Utashi Wako, na ili kukusukuma unipatie hilo ninalokuomba, kwa pendo lile lile la matendo ya kwako.
Lakini, pindi unapozungukia mitaa na miji, panatokea kisa cha kushangaza sana katika makundi yanayokuzunguka Wewe: vipofu, mabubu, viziwi, vilema, waliopooza, wakoma na wenye maradhi na matatizo mbalimbali ya kibinadamu, wanaleta uchungu sana katika Moyo Wako wa Kimungu. Oh, ni jinsi gani unavyotetemeka! Uchungu gani unauelemea Moyo Wako unapoona jinsi hali ilivyogeuka, kuwa matatizo na mahangaiko, na kuwa hali ya kutisha. Ni hali ile ile ya maumbile ya kibinadamu, ambayo hapo awali ilikuwa ni hali nzuri sana, ya kupendeza, na kamilifu wakati ilipotoka katika mikono Yako ya uumbaji. Hayo yote ni matokeo ya utashi wa kibinadamu ulioporomoka na kuharibika. Huo utashi umefurikisha nje yake mambo yake machafu na ukafanya ubinadamu wote upoteze furaha yake.

Lo, Ewe Pendo Langu, ninakuomba kwamba ile FIAT Yako irejee na itawale kati yetu. Kama Wewe ukitaka, unaweza. Na yenyewe FIAT itafukuzia mbali yale matatizo na machungu yote yaliyoletwa na utashi wa kibinadamu. Kwa sababu hiyo mimi ninatiririsha ‘Ninakupenda’ yangu katika tendo lako lile ambapo unafungua macho ya vipofu ili wajipatie tena uwezo wa kuona, ili waweze kuutambua na kuujua Utashi Wako wa Kimungu. Ni vipofu wengi ilioje wa Utashi Wako wa Kimungu! Dunia hii imejaa hawa vipofu duni. Kwa hiyo ninakuomba kwamba wote wapate uwezo wa kuona ili waweze kuutambua na kuutazama Utashi Wako Mtakatifu kabisa.

Lakini natambu, Ewe Pendo Langu, kuwa hatua kwa hatua, unapita kutenda mema mengi kwa watu wale masikini. Anapojitokeza mbele yako yule kiziwi, Wewe, kwa amri ya sauti yako, unamfungulia masikio yake. ‘Ninakupenda’ yangu inatiririkia katika sauti yako inayoamrisha, na pale ninakuomba kwamba ufungue masikio ya wale viziwi wengi wa Utashi Wako wa Kimungu. Katika hatua nyingine, Wewe unafungua ulimi wa yule aliye bubu. Ni bubu wengi wangapi, ambao hawana ulimi tena wa kuweza kuzungumzia ‘FIAT’ Yako ya Kimungu! Na mie hapa, kifudifudi miguuni pako, ninajiegesha penye magoti yako, na ingawa kama ni bado msichana mdogo sana, kamwe sitajitoa hapa mpaka pale utakaponitendea ule muujiza wa kufungua ulimi wa wale bubu wengi, ili hao wote waweze kuzungumzia juu ya Utashi Wako Mwabudiwa. Yesu Wangu, Moyo Wako unaonja dakika za majonzi na maumivu mengi kwa ajili ya mahangaiko ya wanadamu, matatizo yote yakiwa yametokana na utashi wa kibinadamu. Yaelekea sasa unapita kueneza miujiza yako ili kuwakomboa toka matatizo hayo. Tunaomba utujalie neema ya kuuita tena Utashi Wako wa Kimungu ufike kutawala kati ya wanadamu wote. Basi kwa hiyo, uponye na kunyosha viungo vya viwete, uwatakase wakoma, uwaponye waliopooza.

Na mimi, Ewe Mkombozi wa Mbinguni, nitakuwa nikiambatana nawe, nikiwa na hii kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu na Ninakushukuru’. Na je wajua kwa nini ninakupenda, na kwa nini ninakufuata? Ni kwa vile ninapenda unyoshe miguu ya yule anayechechemea katika Utashi Wako, napenda utakase vizazi vya binadamu kutoka ukoma wa utashi wa kibinadamu, ukoma ulioleta ulemavu wa roho na hata ulemavu wa mwili. Napenda uponye wale wengi waliopooza kutokana na utashi wa kibinadamu.

Ewe Pendo Langu, utashi wa kibinadamu ndio uliopanda mbegu ya maovu yote. Kwa sababu hiyo nakuomba utende ule muujiza wa miujiza: kwamba Utashi Wako utawale, hapa duniani kama vile kule Mbinguni ili kwa njia hiyo maovu yote yapate kukoma.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA NANE

Tumfuate Yesu katika matukio mengine ya maisha yake ya hadharani.

Ewe Chema Changu Mpendwa, Wewe unaendelea na maisha yako ya hadharani huku ukiendelea kueneza popote Neno lako la Kimungu, na ukiendelea kuwafariji wale wanaoteseka. Unamsikia mama mmoja anayelia kwa ajili ya mtoto wake aliyefariki, na sasa yupo njiani akienda makaburini kumzika. Mbele ya mama huyo anayelia, Moyo Wako unashindwa kuvumilia kuyaona yale machozi yanayomtoka. Wewe unalijongea jeneza, unayaita yale maiti yaamkie kwenye uzima na unamkabidhi mtoto yule kwa mama yake. Ewe Pendo Langu, ‘Ninakupenda’ yangu haiwezi kukuacha katika tendo lako hili la kutoa uhai kwa mtu aliyekufa. Ninakuomba uziite zile roho nyingi sana, zilizokwisha kufa mbele ya Utashi Wako wa Kimungu, na ufute machozi ya Utashi wako wa Kimungu, ambayo ni machozi yako pia. Utashi Wako, zaidi ya mama yeyote, umekuwa ukilia kwa kipindi cha karne nyingi sana, unapoangalia watoto wake wengi sana wakiwa wamekufa sababu ya kutoishi ndani yake.

Ewe Yesu Wangu, Uhai Wangu Mtamu mno, Pendo Lako linakusukuma uwe unakimbiakimbia huko na kule, kwenda kila mahali. Unapoitwa kumfufua msichana mdogo wewe hukukataa. Kwa mkono wako unamshika mkono wake, na katika tendo la kumwinua juu, unamwita kurejea katika uzima. Unasema: “Msichana huyu hajakufa, bali analala”. Ewe Pendo Langu, ni wengi walioje, ambao wanalala katika usingizi wa utashi wao wa kibinadamu, na mimi ningependa kutiririsha ‘Ninakupenda’ yangu katika tendo lako lile la kunyosha mkono ili kumfufua msichana. Ndipo ninapenda kukuomba, unyoshe mkono wako wa kulia, kuwaita warejee kwenye uhai ndani ya Utashi Wako. Wala hapatakiwi kitu kingine, isipokuwa kuguswa na Mkono Wako wa uumbaji, yaani kuguswa na tendo la Maweza Yako juu ya roho hizo, ambazo zinalala katika usingizi wa utashi wa kibinadamu. Utende hilo sasa kusudi uunde kikosi cha kwanza cha Ufalme wa FIAT Yako ya Kimungu.

Ewe Yesu Wangu Mpole, kuna bado tukio lingine la kushangaza linalokungoja bado: Wanakuja kwako Marta na Magdalena , wakikufuata ili kukutaarifu kuwa kaka yao amekwisha kufariki. Wanalia, na Wewe unashikwa na uchungu hivi, hata unaanza kulia pamoja nao, na unawaomba wakuchukue kwenda kukuonyesha kaburi lake Lazaro. Ulipowasili kaburini, unawaamrisha walifungue kaburi. Ulitazama na kuona kuwa, baada ya siku nne tu mwili wake ulikuwa umeoza, hata hakuweza kutambulikana tena, na wala hakuweza kusogelewa kwani mwili ulikuwa unatoa harufu mbaya. Wewe unatehemu, unatetemeka na kulia machozi, na kwa sauti ya kuamrisha yenye kutetemeka kutokana na uchungu wako mkali, unasema: “Lazaro, amka uje nje!”. Na ndivyo unamfufua.

Ewe Pendo Langu, kwa nini unalia na kwa nini unapata uchungu mkali katika tendo la kumfufua Lazaro? Ndipo Yesu, alinishika na kunibania kwake na mimi nikamshika na kumbana sana ili niweze kusikia mapigo Yake ya Moyo unaoteseka. Mwangwi wa sauti yake ukawa unasikika ndani ya moyo wangu akiniambia: “Binti Yangu Mdogo, huyu Lazaro aliyekufa, kwangu mimi, amekuwa anawakilisha ubinadamu wote uliokuwa umezeekea katika uovu. Kwa utashi wa kibinadamu, ubinadamu umegeuka kuwa ni maiti iliyooza na inayotoa harufu mbaya. Hiyo hali halisi ya maovu yake, imefanya familia nzima ya binadamu iwe inanuka na isiwe inavumilika mbele yangu. Hali hiyo inaniletea machozi, inanifanya nitehemu kwa maumivu. Na wewe tafadhali uwe unalia pamoja nami na uwe unasali”.
Ah, ndiyo, Ewe Uhai wa Moyo Wangu, mimi ninalia pamoja nawe. Maneno yako hayo ya ‘Lazaro, amka uje nje!’, mimi ninataka niyajaze na ‘Ninakupenda’, na ‘Ninakuabudu’, ili kauli hiyo ikushawishi uwe unayarudia rudia juu ya kila moyo. Huku ukiwa unayamwaga machozi yako kama umande uletao baraka, uwe unarudia kusema: “Toka nje ya kaburi hilo la utashi wa kibinadamu, na ebu uingie tena katika uhai wa Utashi wa Mungu”. Kwa minajili hiyo, watakapokuwa wakisikia uamrisho wa sauti Yako, wote waamke na kuuunda Ufalme wa ‘FIAT’ Yako.

Ewe Yesu Wangu Mpendwa, mimi sitakuacha peke yako kamwe. Ingawa kama sijui ni kitu gani cha kukuambia, lakini, angalau ninajua kukuambia ‘Ninakupenda, Ninakupenda’. Ninataka, matendo yako yote, hatua zako, maneno yako, na hata machozi yako yote, niyasuke pamoja na ‘Ninakupenda’ yangu ndogo, na mwishowe nataka nikuombe utupatie FIAT Yako yenye kutawala, na yenye kuamrisha. Kwa sababu hiyo mimi ninakufuata pamoja na wanafunzi wako. Wakati unapolala usingizi pale ndani ya mashuha, ikiwa ni ishara ya pumziko unalotaka kumpatia mtu yule atakayeishi katika Utashi Wako wa Kimungu, dhoruba kali inawatia hofu Mitume, hali inayowafanya wapige kelele wakilia: “Mwalimu, Utuokoe, vinginevyo tutateketea!”. Yesu Wangu, hicho siyo kitu kingine isipokuwa ni dhoruba itokanayo na utashi wa kibinadamu ambao, unapovumisha mawimbi yake ya kutisha na makali katika bahari ya maisha, huwa inatutishia kutuzamisha. Ewe Yesu Wangu Mleta amani, pamoja na Mitume, na kupitia ‘Ninakupenda’ yangu, ninapiga nami kelele kwa nguvu nikisema: “Mwalimu, utuokoe, vinginevyo tutateketea!”. Tafadhali, amrisha hii dhoruba ya utashi wa kibinadamu na uifanye itulie. Kwa nguvu ya amri ile ile uliyoitoa juu ya ile dhoruba iliyowakabili Mitume, sasa upatanishe utashi wa kibinadamu na Utashi wa Kimungu, ili utuwezeshe tupumzike katika mikono ya uhakika ya ‘FIAT’ Yako ya Juu kabisa.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA KUMI NA TISA

Tumfuate Yesu katika tendo lake la kuingia Yerusalemu na tumwombe atupatie ushindi wa Utashi wa Mungu dhidi ya utashi wa kibinadamu. Kishapo tumfuate katika tendo lake la kuweka Sakramenti mbalimbali.

Ewe Chema Changu Mpendwa, ninakuona unageuka na kuelekea Yerusalemu tena. Mimi nanakusindikiza kwa kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’. Lakini, ni uchungu upi ambao Moyo Wako unakosa kuukabili dakika hii? Unapoingia hapa Hekaluni unaona ni jinsi gani watu wanavyoikufuru? Je imekuwa sasa ni soko badala ya kuwa ni nyumba ya Baba Yako? Hapo Wewe unatwaa mijeledi ya kamba kamba, na kwa taratibu na kwa amri ya kimungu unaanza kupita kulia na kushoto, ukipindua juu na chini mambo yao yote, huku ukiwafukuzia nje wote wale wanaolikufuru Hekalu. Kutokana na nguvu ya kitendo Chako cha kuamrisha, hamna hata mmoja anayethubutu kukupinga, bali wote wanakukimbia. Ewe Yesu Wangu, Mtawala wa Kimungu, ‘Ninakupenda’ yangu inaingia na kuzifunika zile kamba za mijeledi ili uzichukue tena kamba hizo kwa ajili ya kuuchapa na kuufukuzia mbali utashi wetu wa kibinadamu, ambao umelikufuru sana Hekalu lako hai, yaani roho zetu. Lo, hebu uuchape mijeledi kabisa, kiasi kwamba usithubutu tena kutawala bali utoe kabisa nafasi na kiti chake cha mamlaka kwa Utashi wa Mungu.

Ewe Mchumba Wangu wa Mbinguni, ‘Ninakupenda’ yangu inakufuata katika tukio lile la kuingia Kwako kwa shangwe katika mji wa Yerusalemu. Mimi ninagonga mhuri wa ‘Ninakupenda’ yangu juu ya yale matawi waliyoshika makundi ya watu, naugonga juu ya nguo zile wanazotandika njiani mbele ya miguu yako, ninaugonga katika zile kelele na mashangilio ya ‘hosana, hosana’ wanayokuimbia hao makundi ya watu. Ninagonga muhuri huo kwa ajili ya kukuomba ulete ushindi wa Utashi Wako. Ewe Mfalme Wangu Mtukufu, hilo Umbo Lako la Mtekaji, la Mshindaji, linaelekea kuniletea habari njema ya furaha. Lo, hebu unifurahishe! Kwa Binti Mdogo wa Utashi Wako, hebu sema hivi: “Utafika Ufalme wa MAPENZI YAKO YATIMIE hapa duniani kama vile kule Mbinguni” . Mimi sitakuacha kamwe bali nitaendelea kukuchosha kwa ‘Ninakupenda’ zangu hadi pale nitakapokuwa nimekushinda na wewe utakapofikia kuniambia: “Binti Yangu, Wewe umeshinda. Ninakuahidia kwamba Ufalme Wake utashuka hapa duniani. Wewe sasa na unifuate Mimi. Pendo Langu lina linaonja hamu ya kusindikizwa nawe. Maadui zangu wametafsiri vibaya hayo makelele ya makundi ya watu wanapoimba ‘hosana, hosana’ na kwa sababu hiyo wanatafuta namna ya kuondoa uhai wangu. Mimi lakini, kabla sijakufa, ninapenda niweke Sakramenti mbalimbali kama kumbukumbu ya mwisho ya Pendo Langu la kina, kwa ajili ya wana Wangu, na kwa ajili ya uhai wa kudumu kati yao. Na wewe utaendelea kuniomba daima hiyo ‘FIAT’ yangu ya Kimungu, katika kila Sakramenti, ili kusudi watu wawe wanajipatia Ufalme Wake”.

Ewe Pendo Langu, naendelea kukusogea na kujibana kwako. Na pindi unapoweka Sakramenti mbalimbali, mimi ninaingiza ‘Ninakupenda’ yangu katika kila ubatizo, ili kwa nguvu ya kauli hiyo, nikuombe ‘MAPENZI YAKO YATIMIZWE’ kwa ajili ya kila mmoja aliyebatizwa. Hiyo ‘Ninakupenda’ yangu ninairudia tena katika Sakramenti ya Kipaimara, ili kukuomba ushindi wa Utashi wako wa Kimungu ndani ya kila mwana-Kipaimara. ‘Ninakupenda’ yangu inakuwa ni muhuri wa Sakramenti ya Mpako Mtakatifu ili kusudi nikuombe, kitendo cha mwisho cha uhai wa kila aliye kufani, na kiwe katika Utashi Wako wa Kimungu. Ewe Yesu Wangu, hiyo ‘Ninakupenda’ yangu, ninaitia katika Sakramenti ya Daraja Takatifu ili nikuombe tupate Mapadre wa Utashi Wako na wa Ufalme wake ndani yao. ‘Ninakupenda’ yangu inaenea hadi ndani ya Sakramenti ya Ndoa Takatifu ili kukuomba Wewe utujalie familia zilizoundwa na kujengwa katika ‘FIAT’ yako ya Kimungu. Hiyo ‘Ninakupenda’ yangu, inapanda hadi ndani ya Sakramenti ya Kitubio ili kukuomba Wewe kwamba kila Kitubio wanachofanya na kiwe ni kifo cha dhambi na uwe ni uhai wa Utashi Wako wa Kimungu ndani yao.
Ewe Yesu, Uhai Wangu, hiyo ‘Ninakupenda’ yangu haitakuacha kamwe kwani itakuwa na Wewe kwa umilele. Kwa sababu hiyo, ninaiweka kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu, Ninakushukuru’ ndani ya kila Hostia ya Sakramenti, katika kila chozi la siri unalolidondosha ndani ya kila Hostia iliyogeuzwa, katika kila tusi na uovu unaotendewa, katika kila fidia unayotoa. Ninaiweka hapo ili, pamoja Nawe, niweze kukuomba kuwa: Ufike Ufalme wa Utashi Wako, hapa duniani kama kule Mbinguni. Ewe, Mpiga-mishale Wangu wa Mbinguni, kutoka katika kila Tabernakulo, uzijeruhi tashi za kibinadamu, eneza minyororo Yako ya Pendo, utumie mbinu zako zote za upenzi ili uweze kuzishinda tashi zote za kibinadamu. Badala yake tunaomba utujalie Utashi Wako, ili kusudi huu utashi wetu ufikie kuwa kitu kimoja na Utashi Wako, na iwe hivyo hapa duniani kama vile kule Mbinguni.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...
SAA YA ISHIRINI

Tumfuate Yesu katika Bustani ya Getsemani na katika maumivu ya Mateso Yake
.

Ewe Yesu Wangu Mteseka, baada ya Wewe kujiweka na kubaki katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, unasambaza uhai Wako katika kila Hostia ili kusudi uweze kushuka na kuingia katika kila moyo, na ili kusudi uwe daima tayari kuwafikia wanadamu mbalimbali wanaokuhitaji. Hilo umelitenda ili kutuambia kwamba: “Mimi sitawaacha bali ninabaki pamoja nanyi nyote, ili kusudi niweze kujenga Ufalme wa Utashi Wangu wa Kimungu kati ya watoto Wangu”. Pendo lako sasa limeridhika. Halafu unaingia katika bahari ya Mateso yako. Hatua za miguu yako zinaelekea kwenye Bustani ya Getsemani. Ninakuona ukianguka kifudifudi ardhini ukisali. Lakini pindi ukisali, unaingia katika mahangaiko na fadhaa, unahema, unaingiwa na maumivu makali sana, na unatoka jasho la damu. Mambo yote yote yanakuja mbele yako. Maumivu yote na dhambi zote, zote zikiwa ni matokeo ya silaha chafu za mauaji zilizopo katika utashi wa kibinadamu ambao unapiga vita dhidi ya Mungu. Ah, ni kweli, utashi wa kibinadamu, kwa kutumia silaha zake, huleta maumivu makali kwa Utashi wa Mungu. Kwa karne nyingi sana utashi huo wa kibinadamu umekuwa ukiuzuia Utashi wa Mungu, na bado unaendelea hata leo kuuzuia. Ewe Yesu Wangu unayekabiliwa na maumivu makali kabisa, huu moyo wangu duni unashindwa kuvumilia unapokuona Wewe umeanguka ardhini na unaogelea na kulowana katika Damu Yako Mwenyewwe. Ni hasa kwa ajili ya hoja hiyo, mimi ninakuomba utupatie Ufalme wa Utashi Wako wa Kimungu hapa duniani, ili kusudi, kwa nguvu ya silaha zake za Kimungu, uweze kuzishinda silaha za utashi wa kibinadamu, uweze kuutesa na kuuingiza katika maumivu makali, hata kuweza, kwa haki kabisa, kulipa kisasi kwa maumivu marefu ya karne nyingi sana, yaliyosababishwa nao huo utashi wa binadamu. Na bila kuupatia tena mwanya wa uhai, Utashi wa Mungu ushike uwanja wake wa uhai katika kila moyo. Na mimi, Ewe Yesu Wangu, ninapokuchukua na kukushika sasa kwa mikono yangu, ninapenda nikutulize kwa kutiririsha kauli yangu ya ‘Ninakupenda, Ninakuabudu, Ninakuheshimu’. Ninaitiririsha katika kila tone la Damu uliyomwaga, katika kila umivu, na katika kila hangaiko na kuhema kwako. Katika kila dhambi unayoiona, ninapenda nitengeneze mawingu ya ‘Ninakupenda’, ili kusudi jicho lako lisiweze kuangalia kitu kingine chochote isipokuwa hiyo ‘Ninakupenda’ yangu. Napenda pia kuwa kila picha chafu na ovyo ya madhambi mengi ifukuziwe mbali kutoka kwako. Naiweka hiyo ‘Ninakupenda’ yangu ili kukuomba kwamba Utashi Wako wa Kimungu utawale hapa duniani.

Ewe Yesu, hebu unisikilize: Kama Utashi Wako ungetawala, Wewe usingejikuta katika maumivu mengi na wala usingepata mateso makali yanayokumaliza namna hii. Kwa sababu hiyo, kabla ya kuondoka toka hapa Bustanini, tafadhali unipe kauli yako, umfurahishe huyu Binti Yako Mdogo na uniambie kwamba ushindi wa Utashi Wako wa Kimungu unafika.
Yesu Wangu Mteseka, maadui zako tayari wamekwisha kuingia hapa Bustanini. Wanakushika na kukufunga kwa kamba na minyororo, wanakukanyaga kwa miguu yao, wanakuburuza, wanakupeleka toka baraza moja la mahakama hadi baraza lingine. Ewe Pendo Langu, mimi ninakufuata hatua kwa hatua, ili juu ya maumivu yako yote nikaweke alama ya ‘Ninakupenda’ yangu na ndivyo niweze kukuomba kwamba, kwa kamba zako na minyororo yako, uufunge utashi wetu wa uasi, ili usithubutu tena kuupinga Utashi Wako wa Kimungu, bali badala yake uuache huru kabisa na kuuruhusu uwe unatawala. Ewe Yesu Wangu, maadui zako wala hawatulii, wanakujaza maumivu makali, wanakutemea mate hata kuziba uso wote. Wanakushitaki kama mhalifu wa jinai, na wanakuhukumu kufa na wanakufunga katika mahabusu. Ewe Mfungwa Wangu Yesu, mimi sitakuacha. ‘Ninakupenda’ yangu inafunika yale mate yote waliyokutemea ili kusudi Wewe usiwe unapata harufu ya mate hayo, bali upate harufu ya ‘Ninakupenda’ yangu. Nataka nikufunike mwili mzima na hiyo ‘Ninakupenda’ yangu ili kusudi katika maumivu yako yote, na katika matusi wanayokutukana, ‘Ninakupenda’ yangu iwe inakutetea na kukulinda, iwe inakunogesha, na iwe ni silaha itakayowafukuza na kuwakimbiza maadui zako na kuwaongoa wote kwa ajili Yako. Na hapo ndani ya gereza hilo jeusi kabisa wanamokufungia, ‘Ninakupenda’ yangu iwe ndiyo mwanga wako na msindikizaji wako anayekuomba utufungulie kutoka gereza la utashi wetu na utufanye sisi kuwa wana huru wa FIAT Yako ya Kimungu.

Ewe Yesu Wangu unayepigwa mijeledi, kwa muda fulani wanakutoa nje ya gereza ili muda huo wao waweze kubadilisha na kukuandalia mateso makali zaidi na ili wafanikishe kutekeleza nia yao ya kikatili ya kukuua. Wanakuburuza na kukupeleka kwenye mabaraza mengine ya mahakama, yaani kwa Pilato na kwa Herode. Huyu Herode ndiye anakudhihaki na kukuchezea hata akakuvalisha kitambaa cha watu vichaa. Tendo hili lilikuletea uchungu mkali usiowahi kusikika. Ewe Pendo Langu, Unapata mateso yalioje! Kwa njia ya ‘Ninakupenda’ yangu, ninataka nikushonee vazi lililoandikwa ‘Ninakupenda’ yangu ya mwanga, ili iwatie kiza hao adui zako, hata wasiweze kukutesa zaidi. Badala yake wawe wanakutambua Wewe na wawe wanakuomba ili utuondolee huu ukichaa wetu ambamo utashi wa kibinadamu umetutumbukiza. Na kwa kutufanya kuwa vichaa, unatufanya tupoteze akili yetu ya kutambua kitu kilicho chema na cha kweli, yaani kutekeleza Utashi Wako wa Kimungu.

Baba yetu...,
Salamu Maria...,
Atukuzwe Baba...